Fei Toto, Manula waitwa Taifa Stars kuzivaa Niger, Morocco

© Azam FC

KANDANDA Fei Toto, Manula waitwa Taifa Stars kuzivaa Niger, Morocco

Zahoro Mlanzi • 14:08 - 07.11.2023

Fei Toto amerudishwa kikosi baada ya kuonesha kiwango bora tangu kuanza kwa msimu huu akifunga mabao manne na asisti zaidi ya mbili katika mechi nane za Ligi Kuu Tanzania Bara.

Wachezaji Feisal Salum 'Fei Toto' na Kipa, Aishi Manula, wameitwa katika kikosi cha timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars), kinachojiandaa na mechi mbili za kufuzu Kombe la Dunia.

Mechi ya kwanza Stars itacheza Novemba 18 dhidi ya Niger na kisha baadaye itaumana na Morocco Novemba 21.

Fei Toto anakipiga ndani ya Azam FC, amerudishwa kikosini baada ya kukosekana kwa muda mrefu hata hivyo ameonesha kiwango bora tangu kuanza msimu huu akiwa amefunga mabao manne katika mechi nane huku akiwa na asisti zaidi ya mbili.

Manula ambaye ndiye Kipa Bora kwa sasa katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, amerudishwa kikosini baada ya kupona majeraha yake ya nyama za paja yaliyomfanya kuwa nje ya uwanja tangu Aprili.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kocha, Adeli Amrouche, mabeki wawili wa pembeni wa timu ya Simba, Mohamed Hussein na Shomari Kapombe, wameendelea kutoitwa katika kikosi hicho licha ya kuwa katika kiwango bora.

Kikosi kamili ni makipa, Beno Kakolanya (Singida FG), Aboutwalib Mshery na Metacha Mnata (Yanga) na Kesi Kawawa (Karlslenden ya Swideni).

Mabeki ni Dickson Job, Bakari Mwamnyeto na Ibrahim Abdullah na Nickson Kibabage (Yanga), Lusajo Mwaikenda na Edward Mwanyama (Azam), Haji Mnoga (Aldershot Town ya England), Abdi Banda (Richards Bay ya Afrika Kusini), Novatus Miroshi (Shakhtar Donetsk ya Ukraine), Edwin Balua (Prisons), Abdulmalik Zakaria (Namungo) na Omary Mvungi (Nantes ya Ufaransa).

Viungo ni Ibrahim Joshua (Tusker ya Kenya), Mzamiru Yassin (Simba), Sospeter Bajana (Azam), Baraka Majogoro (Chippa United ya Afrika Kusini), Mudathir Yahaya (Yanga), Morice Abraham (FK Spartak ya Serbia), Himid Mao (Talaea El Gaish ya Misri) na Ladaki Chisambi (Mtibwa Sugar).

Washambuliaji ni Mbwana Samatta (PAOK FC ya Ugiriki), Saimon Msuva (JS Kabylie ya Morocco), John Bocco na Kibu Denis (Simba), Abdul Suleiman (Azam), Ben Starkie (Basford United ya England), Matteo Anthony (Mtibwa), Clement Mzize (Yanga) na Charles Mmombwa (Macurthur ya Australia).