Gamondi ajivunia kuifundisha Yanga SC

KANDANDA Gamondi ajivunia kuifundisha Yanga SC

Na Zahoro Mlanzi • 21:00 - 06.11.2023

Hii ni miongoni mwa siku zangu bora sana katika maisha ya ufundishaji mpira, ushindi mkubwa dhidi ya wapinzani wazuri, ni nzuri sana kwangu na wachezaji pia

Kocha wa timu ya Yanga SC, Miguel Gamondi, amesema anajivunia kufundisha timu ambayo ina kikosi chenye wachezaji wenye vipaji vya hali ya juu.

Kocha huyo ameyasema hayo baada ya kuibuka na ushindi mnono wa mabao 5-1 dhidi ya watani zao wa jadi, Simba kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara uliofanyika Jumapili Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.

"Ninajivunia kuwa hapa, timu ina wachezaji ambao wana vipaji maridhawa na halisi kwa ajili ya ushindani,' amesema Gamond.

Aidha Gamondi amesema ushindi huo dhidi ya Simba kwenye dabi ni ushindi mkubwa na uliomfurahisha zaidi katika maisha yake ya soka tangu alipoanza kufundisha.

Amesema Simba ni miongoni mwa timu bora na ngumu kufungika kwahiyo kwake kupata ushindi dhidi yao ilikuwa ni ushindi mzuri.

"Hii ni miongoni mwa siku zangu bora sana katika maisha ya ufundishaji mpira, ushindi mkubwa dhidi ya wapinzani wazuri, ni nzuri sana kwangu na wachezaji pia," amesema.

Kwasasa kikosi cha Yanga ambacho kinaongoza msimamo wa ligi hiyo, kinajiandaa na mchezo wao wa Jumatano dhidi ya Coastal Union utakaopigwa Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga ambapo leo wamefanya mazoezi ya 'gmy'.

Tags: